UJUMBE WA KINABII KUHUSU
KUNYAKULIWA KWA KANISA
Kufuatia changamoto za kiimani ambazo jamii ya wanafunzi wa
Yesu Kristo tunazipitia; na kutokana na matishio mbali mbali yanayotishia
uhusiano wetu wa kiroho na Bwana Yesu; ni dhahiri kwamba umefika wakati wa
kuzingatia vipaumbele vya imani ikiwa ni pamoja na kuzingatia ujumbe wa kinabii
kuhusu kunyakuliwa kwa kanisa la Kristo.
Mada hii inaanza kwa kuchambua maana ya misamiati wa
kunyakuliwa, jinsi tukio litakavyokuwa, sababu za kunyakuliwa; na mchakato wa
maandalizi ya unyakuo wenyewe. Karibuni.
MAANA YA KUNYAKULIWA
"Kunyakuliwa" ni tukio maalum la kinabii ambalo
linatarajiwa kutokea wakati wowote kwa ajili ya kuhitimisha huduma za Kanisa la
Kristo duniani. Tukio hili linawahusu makundi mawili ya walengwa. Kundi la
kwanza ni “kufufuliwa kwa wafu waliolala
mauti katika Kristo”! Na kundi
la pili ni “wanafunzi halisi wa Yesu
Kristo tutakaokutwa hai. Na hii ni kwa mujibu wa maandiko ya Paulo
alipowaandikia Wathesalonike:
"Lakini, ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala
mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini. Maana, ikiwa
twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika
Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye. Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno la
Bwana, kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake Bwana,
hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti. Kwa sababu Bwana mwenyewe
atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na
parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi
tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki
Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele. Basi, farijianeni kwa
maneno hayo." (1 THE. 4:13-18)
JINSI UNYAKUO UTAKAVYOFANYIKA
Tukio hili la kinabii litafanyika kwa kasi na kwa
kushtukiza. Hakutakuwepo na taarifa ya kujiandaa kwa unyakuo. Maandiko yanasema
kwamba itakuwa ni: "kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa
parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na
uharibifu, nasi tutabadilika." (1 KOR. 15:52)
Kwa sababu ya kushtukiza kwa tukio hili la ghafla imeandikwa
ya kuwa kuna baadhi waliotakiwa kunyakuliwa wataachwa kwa sababu ni kwa ajili
ya watakaokutwa wako tayari tu ndio watakaonyakuliwa:
"Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo
kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa kama vile siku zile
zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na
kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, wasitambue, hata Gharika
ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Wakati
ule watu wawili watakuwako kondeni; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa; wanawake
wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa.Kesheni basi; kwa maana
hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu." (MT. 24:37-42)
SABABU ZA KUNYAKULIWA
Baada ya kupitia tafsiri na jinsi unyakuo utakavyofanyika,
napenda tupitie hoja muhimu za sababu za kunyakuliwa. Napenda kuzielezea sababu
hizi kwa sababu kuna malumbano ya kitheolojia kuhusu unyakuo na mjadala
ukilenga ni wakati gani unyakuo utafanyika.
Kuna kundi lenye kudai kunyakuliwa kutafanyika kabla kuanza
kipindi cha miaka 7 ya dhidi kuu (Pre-tri-rapture) ; kundi la pili linaamini
unyakuo utafanyika katikati ya kipindi cha miaka 7(Mid-tri-rapture); na kundi
jingine linaamini kunyakuliwa kutafanyika mwishoni mwa dhiki kuu
(Post-tri-rapture)
Uchunguzi wangu na imani yangu vinaangukia katika kundi la
kwanza la(Pre-tri-rapture) na ndiyo maana nimeona nitoe sababu za kunyakuliwa
kabla ya kuanza kipindi cha dhiki kuu.
1. Ahadi ya Yesu Kristo
Yesu mwenyewe ndiye aliyetangulia kuwajulisha wanafunzi wake
kuhusu suala la kurudi tena kuwachukua ili wakae pamoja naye mbinguni: "
Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana
naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja
tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo." (YN. 14:2-3)
2. Kuepushwa na ghadhabu ya Mungu
Mtume Paulo alidokeza habari za ujio wa Mpinga Kristo na
atakavyotawala chini ya uvuvio wa Shetani mwenyewe. Na Kisha akataja habari za
wale watakaochwa baada ya unyakuo watakavyoingia kwenye kipindi cha udanganyifu
mkubwa wa Shetani kwa sababu walikataa kuamini kweli ya Injili kabla ya unyakuo:
“Hapo ndipo
atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake,
na kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake; yule ambaye kuja kwake ni kwa mfano
wa kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; na
katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali
kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa. Kwa hiyo Mungu awaletea nguvu ya upotevu,
wauamini uongo; ili wahukumiwe wote ambao hawakuiamini kweli, bali walikuwa
wakijifurahisha katika udhalimu.”
(2 THE. 2:8-12)
Kwa hiyo, kunyakuliwa kabla ya kipindi cha utawala wa
MpingaKristo ni ili tuepushwe na hii ghadhabu ya Mungu inayotarajiwa kuupata
ulimwengu katika kipindi hicho: “Kwa
kuwa wao wenyewe wanatangaza habari zetu, jinsi kulivyokuwa kuingia kwetu
kwenu; na jinsi mlivyomgeukia Mungu mkaziacha sanamu, ili kumtumikia Mungu
aliye hai, wa kweli; na kumngojea Mwanawe kutoka mbinguni, ambaye alimfufua
katika wafu, naye ni Yesu, mwenye kutuokoa na ghadhabu itakayokuja.” (1 THE. 1:9-10)
TISHIO LA KUACHWA KAMA HAKUNA MAANDALIZI
Kufuatia tukio la kunyakuliwa kufanyika ghafla, ndiyo maana
maandiko yanahimiza walengwa wa unyakuo kuwa tayari wakati wote ili
wasijekuachwa wakati wa unyakuo. Na hii ndiyo sababu ya kuamini kwamba unyakuo
utafanyika kabla ya kipindi cha dhiki kuu ili walengwa wawe wametimiza vigezo
vya unyakuo huo wasijepatwa na mabalaa ya dhiki kuu.
Ushahidi ni maandiko yanayo tahadharisha kuwa tayari, kutubu
na kuishi maisha ya utakaso kamili wakati wote: "Na ndani yake hakitaingia
kamwe cho chote kilicho kinyonge, wala yeye afanyaye machukizo na uongo, bali
wale walioandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo." (UFU. 21:27)
Yesu mwenyewe aliyaonya makanisa ya Karne ya kwanza
yajitakase na kujiweka tayari kwa unyakuo vinginevyo yatakosa fursa hiyo. Kwa
Kanisa la Efeso alilionya akisema: "Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka;
ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako,
nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu." (UFU. 2:5)
Maana ya "Kuondolewa kinara" ni kufutiwa haki ya
urithi wa ufalme wa mbinguni na kufutwa jina kwenye kitabu cha uzima. Mtume
Paulo naye anasisitiza akisema kwa kuwa siku ya unyakuo yaja kama mwivi na
itawakumba wote wasiojiandaa;akasema sisi tusikubali kubaki gizani mpaka
tuvamiwe ghafla:
“Maana ninyi
wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.
Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula,
kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa. Bali ninyi,
ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi.” (1 THE. 5:2-4)
Tutaendelea na sehemu ya pili ambapo tutapitia mchakato wa
maandalizi kwa ajili ya kunyakuliwa, ni mambo gani yatakayojiri baada ya
unyakuo mbinguni na nini kitaendelea duniani. Tafadhali kama ujumbe huu
umekugusa nijulishe kwa ku-like ukurasa huu na kisha warushie na marafiki zako
wengine.
SEHEMU YA PILI
UJUMBE WA KINABII KUHUSU KUNYAKULIWA KWA MANISA
ZIJUE KAMBI ZA NADHARIA KUHUSU UNYAKUO
Kufuatia mwitiko na mrejesho wa makala hii sehemu ya kwanza,
nimelazimika kuwasilisha uchambuzi na tathmini ya kambi za Nadharia kuhusu
unyakuo ambazo kubwa ziko tatu. Moja inafundisha “Unyakuo Kabla ya kipindi cha dhiki kuu” (Pre.tribulation rapture); ya
pili inafundisha “Unyakuo
utafanyika katikati ya Dhiki kuu”
(Mid-tribulation rapture), na ya tatu inafundisha “Unyakuo utafanyika baada ya dhiki kuu” (Post-tribulation rapture).
Nitazitambulisha kwa kifupi na kutoa maoni yangu kwako msomaji wangu mpendwa:
KAMBI YA UNYAKUO KABLA YA DHIKI KUU
UNYAKUO KABLA (PRE-TRI) ni kambi ya nadharia inayofundisha
ya kwamba kunyakuliwa kutafanyika KABLA ya kuanza kwa kipindi cha dhiki kuu.
(Yh.14:1-4; 2 Thes.2:7-12).
Aidha, kambi hii inasimamia maandiko ya: "Maana ile
siri ya kuasi hivi sasa inatenda kazi; lakini yuko azuiaye sasa, hata
atakapoondolewa. Hapo ndipo atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua
kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake..."
(2 Thes.2:7-8)
Kambi hii inatetea msimamo wake kutokana na maneno ya Yesu
aliyoliahidi kanisa la Thiatira kwamba ataliepusha lisiingie kwenye kipindi cha
dhiki kuu (Ufu.3:10)
Kambi hii pia inayatafsiri maneno ya Yesu katika Injili ya
Mathayo Sura ya 24 kuwa ni maonyo ya kinabii kwa ajili ya taifa la Israeli na
majanga yatakayowapa wakati wa dhiki kuu na sio kwa kanisa
KAMBI YA UNYAKUO KATIKATI MWA DHIKI KUU
Kambi hii yenyewe imeamua kusimama katikati na kufundisha ya
kuwa Kanisa lazima lipitie katika dhiki: (Matt. 5:11-12, 10:34-35, 24:1-31;
Mk.13:1-27; Lk 21:1-28; Yh 16:33, 17:15; Yk1:2-15; 1 Pet. 4:12-19).
Kambi hii ya unyakuo kufanyika katikati mwa dhiki kuu ni
utetezi kwamba Kanisa halitashiriki mapigo ya ghadhabu ya Mungu (Lk 21:36). Kwa
hiyo Kanisa litanyakuliwa katikati ya dhiki kuu ili kuepushwa ghadhabu ya Mungu
katika dhiki kuu ((Rum. 5:9; 1 Thes. 1:10, 5:9)
KAMBI YA UNYAKUO BAADA YA DHIKI KUU
Kambi hii ni kongwe na inafundisha ya kwamba Kanisa
litakuwepo katika dhiki kuu na kunyakuliwa mwishoni mwa dhiki kuu ((Matt.
24:29-31)
Msimamo wa kambi hii unasimamia nukuu za maandiko yasemayo: “Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo
dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa,
wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu
yeyote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.” (MT.24: 21-22)
Kisha wanasimamia nukuu za maneno ya “Lakini mara , baada ya dhiki ya siku zile……..ndipo itakapoonekana ishara
yake Mwana wa Adamu mbinguni……nao
watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na
utukufu mwingi…… Naye
atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda, nao watawakusanya
wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu.” (MT. 24:29-31)
Kisha wanatumia nukuu za maneno yasemayo:“…Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii
wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini,
hata walio wateule.” (MT. 24:24)
Kwa mtazamo wa kambi hii msamiati wa neno “wateule”
unatafsiriwa kuwa ni “kanisa”! Wanafundisha ya kwamba: i)
Kanisa litakuwepo duniani kwa kipindi chote cha dhiki ya siku za mwisho, ii)
Kanisa litakutana na upinzani wa Mpingakristo na chapa yake ya mnyama, iii)
Kila mtu duniani, wakiwemo wote wanaomwamini Yesu Kristo, watashinikizwa
kufanya maamuzi ya kukubali au kukataa chapa ya mnyama, iv) Kanisa lazima
lijiandae kwa nyakati ngumu zitakazolikabili kwenye dhiki kuu, v) Kanisa
litanyakuliwa mwishoni mwa dhiki kuu
UCHAMBUZI WANGU KUHUSU KAMBI ZA UNYAKUO
Kwanza naomba nieleweke kwamba miye sio mshabiki wa kambi za
nadharia kwa kufuata mkumbo. Nimefundishwa na kuzoezwa kufanya utafiti binafsi
katika maandiko na kupata tafsiri na matumizi sahihi ya maandiko. Sasa
inapotokea utafiti wangu ukaangukia kati ya moja wapo ya kambi husika, hiyo
haina maana ya kwamba mimi ni mwana-kambi hiyo kwa ushabiki tu.
Kwa mujibu wa kambi za nadhari kuhusu unyakuo, utafiti wangu
umejikuta ukiangukia kwenye kambi ya kwanza ambayo ni “Unyakuo kabla ya kipindi cha dhiki kuu” Nimezifuatilia hoja zao na
tafsiri ya maandiko nikathibitisha ndivyo yalivyo.
Hata hivyo, ilinichukua muda mrefu kujifunza kwa umakini
kuhusu hoja za kambi ya “Unyakuo
baada ya dhiki kuu”
(Post-tribulation rapture) ili kujua usahihi wa kile wanachoamini, chimbuko la
kambi yenyewe na mwelekeo wake kiimani.
Katika utafiti wangu nilikuja kugundua eneo moja kubwa
ambalo viongozi wa kambi hii walighafilika na kutoka nje ya tafsiri sahihi na
hiyo ikazifanya hoja zao zote nazo kupoteza maana yake halisi.
Eneo hilo kutafsiri ya kwamba, kanisa litakuwepo kwenye
dhiki kuu kwa vile limetajwa kwa jina la “wateule” kama tulivyosoma kwenye
baadhi ya nukuu za maandiko.
Uchambuzi wangu katika eneo hilo ni kutumia maandiko hayo
hayo kuthibitisha kwamba “wateule” wanaotajwa kwenye maandiko
husika hayalihusu “kanisa” badala yake yanalihusu “Israeli” kama taifa. Na kama “wateule”
ni “Israeli” na sio “kanisa” dhana nzima ya kunyakuliwa
baada ya dhiki kuu inapoteza uhalali wake kimaandiko. Hoja zangu za utetezi ni
kama ifuatavyo:
1. Mjadala wa mazungumo ulihusu taifa la Israeli
Katika Mathayo 24: Yesu alikuwa anajibu maswali ya wanafunzi
wake kwa mtazamo wa Israeli kama taifa na sio kwa mtazamo wa kanisa. Ushahidi
ya kwamba aliongea nao kwa mtazamo wa Israeli badala ya kanisa ni maneno yake
ya: “ hapo mtakapoliona chukizo la
uhabiribu….limesimama katika patakatifu……ndipo walio Uyahudi na
wakimbilie milimani…”
(MT.24:15-16)
2. Kipaumbele cha huduma ya Yesu kilikuwa ni Israeli
Yesu mwenyewe alikwisha kujitambulisha kwamba ujio wake na
huduma yake kipaumbele chake kilikuwa ni kwa taifa la Israeli na sio mataifa: “Akajibu, akasema, sikutumwa
ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (MT.15:24). Na sio kwamba kipaumbele chake ni kwa
Israeli kama taifa tu, hata alipowatuma wanafunzi wake ambao wote walikuwa ni
wayahudi hakuwapa ruhusa kutembelea watu wa mataifa: “Hao Thenashara Yesu aliwatuma, akawaagiza, akisema,
katika njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wo wote wa Wasamaria msiingie.
Afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (MT.10:5-6)
3. Katika Ufunuo, Kanisa halitajwi kabisa kwenye kipindi
chote cha dhiki kuu
Katika sura tatu za kwanza za kitabu cha ufunuo, Kanisa
limetajwa mara kumi na tisa lakini kuanzia Sura za 4-18 ambamo tunasoma taarifa
za kina za kipindi cha miaka 7 ya dhiki kuu kanisa halitajwi humo hata mara
moja.
Kana kwamba hii haitoshi, kwenye sura ya 3:10 tunakuta Yesu
alikwisha kuliahidi kanisa ya kwamba ataliepusha lisiingie kwenye saa ya
kujaribiwa kwa ulimwengu: “Kwa kuwa
umelishika neno la subira yangu, mimi name nitakulinda, utoke katika saa ya
kuharibiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi.”
MWELEKEO WA UNYAKUO KABLA YA DHIKI
Unyakuo wa kanisa kabla ya kipindi cha dhiki kuu ndipo Yesu
anapotimiza ahadi ya kuturithisha ufalme wa mbinguni na kuwa pamoja naye
mbinguni (Yh.14:1-3) Kunyakuliwa kunajumisha: i) Waliokufa katika Kristo
kufufuliwa (1 Thes.4:13-16), ii) Tuliosalia kuvalishwa miili mpya na
kunyakuliwa mawinguni (1 Thes.4:17), iii) Kukutana kwenye Kiti cha hukumu cha
Kristo kwa ajili ya thawabu mbinguni (2 Kor.5:10), iv) Kushikiri karamu ya
arusi ya Mwanakondoo mbinguni (Mt.26:29; Ufu.19:7-9)
Bado mada inaendelea. Najua uchambuzi wangu umetibua sana
mitazamo ya kambi ya nadharia za unyakuo. Mimi simo kwenye kambi hata moja ila
ninasimamia tafsiri sahihi ya maandiko ambayo yamekuwepo kabla ya kambi za
nadharia zilizopo.
Sehemu inayofuata nitaendelea kufafanua ni kwanini “kambi ya unyakuo baada ya
dhiki” inasimamia kwamba “wateule” ni “kanisa’’ na sio “Israeli”
hata kama maandiko yenyewe wanayosimamia sivyo yasemavyo. Kama umeguswa na mada
nisaidie kwa ku-like post hii na kisha uwarushie na marafiki zako. Ubarikiwe
sana.
SEHEMU YA TATU
UJUMBE WA KINABII KUHUSU KUNYAKULIWA KWA MANISA
Kwenye sehemu ya pili ya mada hii nilisimulia habari za
kambi za nadharia za unyakuo pamoja na imani yangu. Niliahidi katika sehemu ya
kuchambua ni kwanini “kambi ya
unyakuo baada ya dhiki” inasimamia
kwamba “wateule” ni “kanisa’’ na sio “Israeli”
hata kama maandiko yenyewe wanayosimamia sivyo yasemavyo. Lakini kutokana na
mrejesho niligundua kuwepo kwa utata wa kuchanganya matukio mawili tofauti kuwa
tukio moja. Katika sehemu hii ya tatu nimeona nitoe ufafanuzi na kisha kudokeza
kuhusu hatari ya mtazamo wa madai ya kanisa kuwepo kwenye dhiki kuu:
ZIJUE TOFAUTI KATI YA "KUNYAKULIWA
KANISA" NA "YESU KURUDI MARA YA PILI"
Unyakuo na kurudi mara ya pili ni matukio mawili tofauti
japokuwa yote ni matukio ya siku za mwisho na yote yanamlenga Yesu mwenyewe.
Kuna utata katika kupambanua baadhi ya maandiko kama yana maana ya unyakuo au
Yesu kurudi mara ya pili dunia.
Tukio la Unyakuo ni wakati Yesu Kristo anakuja kulichukua
kanisa kutoka duniani kwenda mbinguni kama ilivyoandikwa katika (1 Thes
4:13-18; 1 Kor. 15:50-54.) Waliokufa katika Kristo watafufuliwa na tulio hai
tuliosalia tutabadilishwa miili na kunyakuliwa ili kumlaki Bwana mawinguni. Kwa
maelezo mengi unyakuo unalenga kanisa tu. Lakini wakati wa Yesu kurudi mara ya
pili duniani, walengwa ni taifa la Israeli na hukumu dhidi ya mataifa
yatakuwepo duniani kwa wakati huo, kufuta uovu na kusimika utawala wa milenia
duniani (Rev.19:11-16; )
1. Wakati wa unyakuo watakatifu (kanisa) tunakutana na Bwana
mawinguni (1 Thes.4:17). Wakati Yesu anaporudi mara ya pili duniani anakuja
pamoja na watakatifu wake (kanisa) (Ufu. 19:14).
2. Wakati tukio la unyakuo Litafanyika kabla ya dhiki kuu (1
Thes.5:9; Ufu. 3:10). Tukio la Yesu kurudi mara ya pili duniani litafanyika
baada ya dhiki kuu (Ufu 6-19)
3. Tukio la unyakuo linafanyika kuwaepusha watakatifu
(kanisa) na dhiki kuu (1 Thes. 4:13-17, 5:9). Wakati Yesu kurudi kwake mara ya
pili duniani ni kwa ajili ya kuwaokoa wayahudi na kuyahukumu mataifa yote
yaliyokuwa upande wa Mpingakristo (Mat.24:40-41).
4. Tukio la unyakuo litakuwa ghafla na siri (1 Kor.
15:50-54). Wakati Yesu atakaporudi mara ya pili duniani kila jicho litamwona
(Ufu. 1:7; Mat. 24:29-30).
5. Kurudi kwa Yesu duniani mara ya pili ni tukio
litakalofanyika baada ya matukio kadhaa yaliyotabiriwa kufanyika katika siku za
mwisho (2 Thes. 2:4; Mat.24:15-30; Ufu. 6–18).
Lakini unyakuo ni tukio linalotarajiwa kufanyika wakati wowote kuanzia hivi
sasa (Tit.2:13; 1 Thes. 4:13-18; 1 Kor. 15:50-54).
HATARI YA KUAMINI KANISA
LITAKUWEPO DUNIANI WAKATI WA DHIKI
1. Madai ya kwamba kanisa litakuwepo duniani kwenye dhiki
kuu yanakinzana na agizo la Yesu la kuhubiri Injili kwa kila kiumbe ili
aaminiye na kubatizwa ataokoka na asiyeamini atahukumiwa (MK.16:16) Kwa maana
katika kuamini injili mtu anapata ahadi ya uzima wa milele ambayo kilele chake
ni kuingia mbinguni; na asiyeamini anakuwa chini ya hukumu ya milele kwenda
jehanamu ya milele
2. Madai ya kwamba kanisa litakuwepo duniani kwenye dhiki
kuu mpaka mwisho yanakinzana na Ahadi ya Yesu Kristo kwa wanafunzi wake kuwa
kaenda kuwaandalia mahali mbinguni na kisha "atarudi tena kuwachukua"
ili alipo yeye mbinguni na wao wawepo pamoja naye (YH.14:1-3;1 Thes.4:17).
3. Madai ya kwamba kanisa litakuwepo duniani kwenye dhiki
kuu mpaka mwisho yabatilisha unabii kwa kanisa kukusanyika mbele ya Kiti cha
hukumu cha Kristo kwa ajili ya kupokea thawabu na taji za utukufu kwa ajili ya
utumishi wao katik Kristo walioufanya wakiwa hai duniani.( 2Kor.5:10)
4. Madai ya kwamba kanisa litakuwepo duniani wakati wote wa
dhiki kuu yanamfanya Mungu akiuke neno lake la kutokuwahukumu wenyehaki na
waovu pamoja. (1 Thes.1:10; Ufu.3:10) Dhiki kuu ni hukumu ya Mungu ya kuifanya
Israeli imkubali Masihi waliyemkataa (Yer.30:7) na kisha kuyahukumu mataifa
yaliyokubali chapa ya mpingakristo wakati wa dhiki kuu. (Mt.25:32-34)
5. Madai ya kwamba kanisa litakuwepo duniani wakati wa dhiki
kuu kunadhoofisha imani ya kujikana nafsi na kuishi maisha ya utakatifu
duniani. Maana faraja ni matumaini ya kuingia mbinguni; “Kisha sisi tulio hai tuliosalia, tutanyakuliwa
pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja
na Bwana milele. Basi farijianeni kwa maneno hayo. (1 Thes.4:17-18)
Tukutane kwenye sehemu ya nne. Kama umeguswa na mada
nisaidie kwa ku-like post hii na kisha uwarushie na marafiki zako. Ubarikiwe
sana.
SEHEMU YA NNE
UJUMBE WA KINABII KUHUSU KUNYAKULIWA KWA MANISA
UFAFANUZI KUHUSU WATEULE KATIKA MATHAYO 24 NI AKINA NANI
Kambi za nadharia kuhusu unyakuo wa kanisa zina malumbano ya
karne nyingi kuhusu tafsiri ya msamiati wa neno “wateule”
waliotajwa na Yesu Kristo kwenye maandiko ya Injili ya Mathayo 24. Maandiko
hayo kama ifuatavyo:
"Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye
yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo." (MT.24:22);
"Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa
ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio
wateule." (MT. 24:24); "Naye atawatuma malaika zake pamoja na sauti
kuu ya parapanda, nao watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu
wa mbingu mpaka mwisho huu." (MT.24:31; Isa 11:12)
Kwa mujibu wa “kambi
ya nadharia ya Kanisa litapitia dhiki kuu”
(Post-tribulation rapture) wao wanatafsiri kwamba “wateule”
wanaotajwa katika dhiki kuu ni kanisa na sio Israeli. “Kambi ya nadharia ya unyakuo kabla ya kipindi cha
dhiki kuu” (Pre-tribulation rapture)
wanasema “wateule” wanaotajwa hapa ni “Israeli”
na sio “kanisa” kwa kuwa litakuwa limekwisha kunyakuliwa kabla ya
dhiki kuanza.
VIGEZO VYANGU VYA UCHAMBUZI
Kama nilivyokwisha kutoa msimamo wangu huko nyuma na hapa
narudia tena kuthibitisha ya kwamba, mimi si mshabiki wa kambi za nadharia kwa
sababu zote zimeibuka baada ya maandiko yanayobishaniwa yalikwisha kuwepo.
Vigezo vya uchambuzi ninavyotumia vinazingatia ukweli wa mambo yafuatayo:
Kwanza, nachunguza ni wakati gani maneno yalioandikwa
yalisemwa na ni katika mazingira gani ya wakati huo. Kwa sababu wakati maneno
yaliposemwa sio kwamba ndio wakati huo huo yalipoandikwa! Kuna wakati tofauti
kati ya "kusemwa maneno" na wakati "maneno hayo
yalipoandikwa"!
Pili, nani walengwa wakuu wa maneno yaliyosemwa kwa wakati
huo (wayahudi au mataifa?) Hapa pia nazingatia utamaduni wa lugha iliyotumika
na jamii ya wakati huo (kiebrania, kiaramu au kiyunani, kilatini nk)
Mantiki ya kuzingatia lugha iliyotumika wakati maneno
yaliyosemwa ni kwa sababu lugha iliyotumika kusema maneno husika sio lugha hiyo
hiyo ndiyo iliyotumika katika kuyaandika maneno hayo!
Tatu, ni akina nani waliohusika kutafsiri maandiko kutoka
lugha asilia iliyotumiwa na waandishi asilia kuja kwenye lugha nyingine! Mfano
toka Kiebrania kuja Kilatini au Kiingereza; toka Kiyunani kuja Kiingereza. Pia
ni wakati gani kazi ya kutafsiri ilifanyika na kwenye mazingira gani ya
kihistoria.
Mwishoni kabisa ndio nakuja kwenye kuzichambua "kambi
za shule za nadharia" kuanzia chimbuko la kila nadharia husika kihistoria
na kiitikadi. Kwa hiyo utakapoona majibu yangu yakaangukia kwenye msimamo wa
mojawapo ya kambi za nadharia nisihukumiwe kwamba miye ni mfuasi wa nadharia
hiyo.
Na sasa naanza kutoa uchambuzi wangu kuhusu “wateule” waliotajwa kwenye Injili ya Mathayo 24 ni akina
nani? Ni kanisa au Israeli?
WATEULE NI ISRAELI NA SIO KANISA
1. Yesu alitumwa kwanza kwa Israeli kabla ya Kanisa
Mwenye kunishawishi kwa 100% niamini kuwa “wateule”
wanaotajwa kwenye MT 24 ni “Israeli’ na sio “kanisa”
ni maneno ya Yesu mwenyewe kama alivyojieleza kwenye Injili hiyo hiyo ya
Mathayo. Yesu anawataja walengwa wake wakuu wakati wa kipindi chote cha huduma
yake akisema: “……Sikutumwa
ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. “ (MT. 15:24)
Na hata wakati anawatuma wanafunzi wake kwenda kuhubiri kwa
mara ya kwanza aliwapa masharti ya kutokwenda kwa mataifa mengine, wala kwa
wasamaria: “Hao Thenashara Yesu aliwatuma,
akawaagiza, akisema, Katika njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wo wote wa
Wasamaria msiingie. Afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba
ya Israeli. (MT.10:5-6)
Kwa mantiki hii, ni dhahiri ya kwamba maneno ya Yesu
aliyokuwa kwenye mistari inayotaja “wateule” walengwa wake ni “Israeli” na sio “Kanisa”
2. Dhiki iliyotajwa na Yesu katika Mathayo 24 inahusu
Israeli na sio kwa kanisa
Kama nilivyothibitisha hapa juu ya kwamba walengwa wakuu wa
Yesu ni “Israeli” na sio “kanisa”; majibu hayo yanaendelea hata
kwenye kipengele cha walengwa wa dhiki kuu. Mjadala wenyewe unaanzia kwenye
jengo la hekalu. Wanafunzi walipomwonyesha hekalu naye aliwajibu bila kumung’unya maneno akisema:
“ …..Hamyaoni
haya yote? Amin, nawaambieni, Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo
halitabomoshwa. Basi hapo mtakapoliona chukizo la uharibifu, lile lililonenwa
na nabii Danieli, limesimama katika patakatifu (asomaye na afahamu), ndipo
walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani;”
(MT. 24:2,15-16)
Maneno ya unabii wa Danieli yalitaja moja kwa moja kuwa
dhiki italipata taifa la Israeli pamoja na mji wake Yerusalemu (Dan.9:24) Na
Yesu mwenyewe anasisitiza kiunabii akisema ikiwafika dhiki “walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani.”
Na mahali pengine Yesu anasema kwa kuwahurumia: “Ombeni, ili kukimbia kwenu
kusiwe wakati wa baridi, wala siku ya sabato.”
(MT.24:20)
Kwa kifupi, mazungumuzo kati ya Yesu na wanafunzi wake yenye
misamiati ya maneno ya “injili ya
Ufalme (24:14), patakatifu (24:15, na sabato (24:20) yote hii inalenga taifa la
Israeli na sio kanisa.
Nabii Yeremia yeye alifunuliwa na kuipa jina dhiki kuu hiyo
kuwa ni “taabu ya Yakobo”: “Ole! Maana siku ile ni kuu, hata hapana inayofanana
nayo, maana ni wakati wa taabu yake Yakobo; lakini ataokolewa nayo. “(YER.30:7)
KANISA HALIKUWEPO WAKATI HUO KWENYE MATHAYO 24
Madai ya kwamba “wateule” waliotajwa katika Mathayo 24
ni “kanisa” na sio “Israeli” ni dhana ya kufikirika bila
ushahidi kamili.
Ifahamike ya kwamba, Yesu Kristo alikwisha kusema msamiati
kuhusu “kanisa” kwenye Injili hiyo hiyo ya Mathayo. Alipowahoji
wanafunzi wake wanamtambua kama nani na Petro akajibu kuwa ni Mwana wa Mungu
Aliye Hai ndipo Yesu alitabiri habari za ujio wa kitu alichokiita “kanisa”: “Nitalijenga
kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda..” (Mat.16:18).
Muktadha wa msamiati wa lugha kuhusu "kanisa"
linalotajwa hapa unalilenga kitu “kitakachokuwepo
baadaye” na sio kwamba ni kitu
kilichokuwepo kwa wakati huo! Sehemu ya pili ambayo Yesu alitumia msamiati wa
neno "kanisa" ni kuhusu mchakato wa kusamehe na kupatana
utakaozingatia mara kanisa litakapokuwa limeanza hapo baadaye:
“....na
asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikilzia kanisa pia, na awe
kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru”
(Mat.18:17). Maneno haya yoye hayakulenga kuwepo kwa kanisa kwa wakati huo kwa
sababu lilikuwa halijakuwepo bado. Yalikuwa ni maelekezo ya Yesu yatakayotumika
baadaye.
Kama "wateule" waliotajwa kwenye Mathayo 24
wangelikuwa ni "kanisa" Yesu asingemung'unya maneno angelitaja moja
kwa moja kuwa "wateule" hao ni "kanisa"! Lakini kama Yesu
hakusema ni "kanisa" maana yake tafsiri ya "wateule" hao
sio kanisa.
Kwa mantiki hii maneno mengi yaliyosemwa na Yesu walengwa
wake wakuu walikuwa ni kwa Israeli ya Agano la kale na sio Agano Jipya, kwa
sababu hata mazingira ya kihistoria ambamo Yesu alikuwa akihudumu yalikuwa ni
katika kipindi cha Agano la Kale chini ya torati ya Musa na hekalu ibada za
kiyahudi. Agano Jipya limeanza rasmi baada ya kusulubiwa msalabani kufa na
kufufuka kwake. Kwa hiyo kabla ya kifo na kufufuka kwa Yesu kanisa halikuwepo.
Sehemu itakayofuata nitajibu kuhusu swali tata la watakatifu
katika dhiki kuu ni akina na wanatokana na nini? Ni kanisa ambalo
halijanyakuliwa au ni Israeli au ni jamii nyingine? Ikiwa mada hii imekubariki
nijulishe kwa ku-like na warushie marafiki zako pia. Ubarikiwe sana.
SEHEMU YA MWISHO
UJUMBE WA KINABII KUHUSU KUNYAKULIWA KWA KANISA
UTANGULIZI
Nimesoma michango ya majibu ya wasomaji pamoja na maswali
maswali mbali mbali yaliyoulizwa. Maswali yote yaliyoulizwa kwenye sehemu ya
nne yameulizwa nje ya mada. Ninaheshimu michango yote iliyotolewa kwa sababu
kila utu wa mtu ni mawazo yake na ustaarabu kuheshimu mawazo ya mtu. Hata hivyo, maelezo yangu yote yalijikita
katika kujibu kile ambacho Mathayo 24 iliandika kuhusu WATEULE kama ni KANISA
au ISRAELI. Nilionesha maaelezo ya Yesu mwenyewe jinsi alivyosema kuwa alikuwa
anaongea na taifa la Israeli na kwamba kanisa kwa muda huo lilikuwa
halijakuwepo. Kwa yeyote asiyekubaliana na ukweli huu hilo ni suala la
kimapokeo zaidi lakini si la tafsiri sahihi ya kibiblia.
Hii ni sehemu ya mwisho kuhusu mada hii. Yakiwepo maswali
ynayolenga mfululizo wa mada hii tangu mwanzo ambayo msomaji anaona
haijaeleweka nitakuwa tayari kujibu kwa kifupi kabla ya kufungua mada mpya.
Vinginevyo nimesukumwa kuandika kitabu kinachohusu mada hii na kitakapokamilika
msomaji wa ukurusa huu utakuwa wa kwanza kupata habari zake. Kwa sasa napenda
kufunga mada hii kwa kuelezeka kwa mukhtasari tu kuhusu habari za DHIKI na
mchakato wa mambo yakayojiri siku za mwisho:
TAFSIRI YA DHIKI KINABII
Taabu ya uchungu uliokithiri; mateso makali kupindukia;
mazingira magumu yasiyovumilika. Dhiki ni kipindi ambacho ghadhabu ya Mungu
itamwagwa juu ya ulimwengu uliomkataa Mungu kwa kipindi kirefu tangu alipomtuma
Mwanawe Yesu Kristo kwa ajili ya wokovu wa ulimwengu. Walimwengu walichagua uongo
badala ya kweli na kuzidi katika uovu sugu kwa karne nyingi. Mungu alikuwa
mvumulivu kwao kwa muda mrefu na sasa uvumilivu wake utafikia ukomo.
"Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo
haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo
kamwe. Na kama siku hizo
zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule
zitafupizwa siku hizo." (MT. 24:21-22)
"Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye
upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake
haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo; na wakati huo watu
wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu
kile." (DAN.12:1)
KUSUDI LA DHIKI KUU
Kusudi kubwa la kipindi cha dhiki ni kuliandaa taifa l
Israeli kumkubali Masihi ambaye walimkataa wakati alipokuja kwao kwa mara ya
kwanza. Kama ilivyoandikwa ya kwamba: “Alikuja
kwa walio wake lakini hawakumpokea, bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa
kufanyika watoto wa Mungu”.(YH.1:11-12)
Kwa Israeli kumkataa Masihi, fursa ya neema ikapelekwa kwa Mataifa mpaka mpaka
muda wake utakapokamilika (Rum.11:25-27)
Kipindi cha dhiki kimetafsiriwa kiunabii kuwa ni “wakati wa taabu ya Yakobo
(Yer.30:7) kwa sababu ni wakati ambapo Mungu anashughulika na taifa la Israeli.
Huu ndio wakati uamsho wa kiroho kwa wayahudi utasambaa kila kona ya dunia.
Wengi watamwamini Yesu na kuanza kuandaa kizazi kipya cha Israeli watakaoingia
kwenye utawala wa milenia. Mungu atatimiza unabii wa juma moja ili kutimiza
kusudi lake kuhusiana na Israeli (Dan.9:24)
Ni wakati wa dhiki hata mataifa wasio wayahudi nao
watamwamini Yesu kupitia Injili ya Ufalme itakayohubiriwa na wale wayahudi
144,000. Hawa mataifa watakaookolewa wakati wa dhiki kuu na ambao hawatakufa
kwenye dhiki ndio watakajumuika kama kondoo kwenye hukumu ya Kristo kama
ilivyotabiriwa kwenye Mathayo 24.
Kusudi la pili la dhiki ni Mungu kumwaga ghadhabu yake juu
ya walimwengu ambao waliikataa Injili wakati wa kipindi cha kanisa la Kristo
kabla ya dhiki kuanza. Wengi wakati huu watakuwa wamejisajili chini ya utawala
wa Mpingakristo na kushikiri maovu yaliyokithiri na ghadabu ya Mungu atashuka
kwa ajili yao ili kupatiliza maasi yatakayokuwa yakiendelea kila mahali duniani
kwa wakato huo. (2 Thes.2:11-12) Kusudi la tatu la dhiki ni kufanya hukumu
dhidi ya kanisa lililokengeuka ambalo litakuwa likiongozwa na Nabii wa uongo
(Ufu.17:6) Ufu.17:15-18
MCHAKATO WA MAMBO KATIKA DHIKI
Baada ya kunyakuliwa kwa Kanisa, na utendaji wa Roho
Mtakatifu kutoweka juu ya uso wa dunia hii, ndipo ukengefu wa kiimani na
mmomonyoko wa maadili utakithiri kupindukia. Kiwango cha uasi dhidi ya mamlaka
zilizoko kitapanda na kupoteza amani ya kijamii na uhuru wa kuabudu Mungu wa
kweli utatoweka katika jamii. Uvunjwa wa amri za Mungu katika Biblia utakuwa
ndio mtindo wa maisha ya kila siku katika jamii. Wakati huo hakuna tena Injili
ya wokovu kwa kuwa aliyekuwa mtetezi wake hayupo tena duniani. (Hivi sasa yuko
azuiaye)
Kutokana na mkenguko mkubwa wa kiimani na kimaadili katika
dunia nzima, Shetani atatumia fursa hiyo kumtambulisha wakala wake ambaye ni
Mpingakristo ambaye atajitokeza kuwa ni mpatanisha na mtatuzi wa matatizo ya
kisiasa, kiuchumi na kidini ambayo yatakuwa yanasumbua dunia nzima. Huyu Mpinga
Kristo atavuviwa na shetani katika kufanya hata miujiza ya uongo ili
kuwadanganya walimwengu ambao waliikataa Injili ya kweli wakati kanisa la kweli
la Kristo lilipokuwa bado liko duniani. (2 Thes.2:9-10)
Mojawapo ya miujiza mikubwa atakayofanya huyu Mpingakristo
ni kufanikisha zoezi la kusaini mkataba wa Amani kuhusu mgogoro sugu wa
Mashariki ya Kati, kati ya Israeli na Waarabu. (Dan.9:27) Mojawapo ya ushawishi
wake kwa Israeli ni kukamilisha hitaji la ujenzi wa Hekalu la kiyahudi na
wayahudi wataanza kutoa dhabihu za wanyama kama zamani. Na pia atafanikisha
zoezi la kuundwa kwa serikali moja ya ulimwengu mzima ambapo mamlaka za mataifa
binafsi yatajumuishwa pamoja chini ya utawala wa mfumo wa serikali moja ya
dunia.
Wakati huo atatokea mtu mwingine mwenye ushawishi mkubwa
katika mambo ya uchumi na dini (Ufu.13:11-17) Kazi ya mnyama huyu kwa jina
maarufu la Nabii ya uongo atakuwa mpiga debe wa Mpingani Kristo katika
kuhamasisha ulimwengu kumwabudu Mpingakristo sawa na Mungu. Atafanya ushawishi
mkubwa kwa njia ya kuweka mfumo mmoja wa uchumi ambapo kila raia duniani
atawajibika kujisajili kwenye mfumo huo ilia pate kufanikisha mambo yake ya
kiuchumi.
AWAMU YA PILI YA DHIKI
Baada ya kipindi cha miaka mitatu na nusu ndipo awamu ya
pili ya dhiki itaanza kwa Mpingakristo kuvunja mkataba wa amani aliofanya
Israeli na waarabu. Mkataba huo utavunjwa kwa Mpingakristo kuingia kwenye
hekalu na kujitangaza kuwa yeye ndiye Mungu na wayahudi wamwabudu yeye. Hilii
ndilo linaitwa “chukizo la
uharibifu” (Dan.9:27; 2 Thes.2:3-10)
Hii awamu ya pili ya dhiki ndiyo inaitwa DHIKI KUU,
(Ufu.7:14) na ndiyo inaitwa “wakati wa
taabu ya Yakobo (Yer.30:7) Kilele cha dhiki kuu kitafikiwa pale ambapo
Mpingakristo ataongoza vita ya kuiangamiza Israeli kuanzia Yerusalemu maarufu
kwa jina la VITA YA ARIMAGEDONI. Kabla ya kutimiza mkakati huo ndipo Yesu
Kristo mwenyewe ataamua kurudi mara ya pili duniani na majeshi yake ya Mbinguni
na kuja kumwangamiza Mpingakristo na majeshi yake na kuwatupa kwenye ziwa la
moto (Ufu.19:11-21)
Kazi ya Yesu pia itakuwa ni kumkamata Shetani mwenyewe na
kumfunga kwenye shimo la giza kwa kipindi cha miaka 1000 (Ufu.20:1-6); na kisha
Yesu kuweka utawala wa milenia, na makao makuu yakiwa jijini Yerusalemu.
Nachukua fursa hii kuwashukuru wote mliofuatilia mada hii na
kujibu kwa njia mbali mbali. Natarajia kwamba tutaendelea kuelimishana kwenye
mada mpya zinazokuja mbeleni. Mbarikiwe sana.
Comments
Post a Comment